Monday 8 August 2016

OBREY CHIRWA BONGE YA MCHEZAJI

Image result for obrey chirwaKOCHA Mkuu wa Yanga, Hans van Pluijm amesema Obrey Chirwa ni bonge la mchezaji ambaye anahitaji mtu mwenye kasi kama yake ili kuendana naye katika ufungaji magoli.
Pluijm alisema hayo juzi Dar es Salaam baada ya mchezo wa kirafiki kati ya Yanga dhidi ya Mtibwa Sugar waliotoka sare ya bila kufungana.
Alisema Chirwa alionesha kiwango bora katika mchezo huo isipokuwa udhaifu ulionekana hasa baada ya kukosekana kwa mchezaji mwenye mbio sawa na zake na matokeo yake nafasi nyingi alizokuwa akizitengeneza mchezaji huyo zilikuwa zikipotea.
Mchezaji huyo aliyejiunga na Yanga msimu huu akitokea FC Plutinum ya Zimbabwe amekuwa akipangwa katika mechi mbalimbali sambamba na mshambuliaji Donald Ngoma ambaye hakuwepo katika mchezo wa juzi. Kocha huyo aliwapumzisha baadhi ya wachezaji tegemeo kwa ajili ya maandalizi ya mchezo ujao wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Mo Bejaia.
“Chirwa ni mchezaji mzuri mwenye kasi ambayo akipata mwenzake wa kuendana naye watafanya vizuri,” alisema.
Akizungumzia mchezo huo, alisema Mtibwa Sugar imekuwa ikicheza mchezo wa kujihami zaidi.
Kwa upande wake, Kocha wa Mtibwa Sugar Salum Mayanga alisema amegundua kikosi chake kina upungufu katika nafasi ya kiungo, hivyo mchezo huo umemuonesha kasoro anayohitaji kuifanyia kazi.
Yanga inatarajiwa kuingia kambini leo kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Mo Bejaia utakaochezwa mwishoni mwa wiki hii.

No comments:

Post a Comment