Wednesday 10 August 2016

PLUIJM AWAFUNGIA NIYONZIMA NA BUSUNGU

Image result for hans pluijmKOCHA Mkuu wa Yanga, Hans van Pluijm amewafungia kazi wachezaji Haruna Niyonzima na Malimi Busungu kwa kuwapa mazoezi maalumu kwa ajili ya kuwakabili MO Bejaia ya Algeria.
Yanga itacheza na MO Bejaia mwishoni mwa wiki hii kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam, ukiwa ni mchezo wa kundi A wa Kombe la Shirikisho Afrika huku wenyeji wakisaka ushindi wa kwanza baada ya kupoteza mechi tatu na kutoka sare mchezo mmoja.
Katika mazoezi ya jana asubuhi, kocha Pluijm alionekana akiwazidishia dozi wachezaji hao wawili kwa kuwapa mazoezi magumu huku wachezaji wengine wakifundishwa na kocha msaidizi Juma Mwambusi.
Baada ya mazoezi hayo kumalizika, kocha Pluijm aliliambia gazeti hili kuwa ameamua kuwaandaa wachezaji hao kwa sababu walikuwa majeruhi kwa muda mrefu na sasa wamerudi ndiyo maana anawaandaa kwa ajili ya mechi zinazokuja, ikiwemo ile ya Jumamosi dhidi ya MO Bejaia.
Mshambuliaji Donald Ngoma ataukosa mchezo huo wa Jumamosi kutokana na kuwa na kadi mbili za njano na nafasi yake inaweza kuchukuliwa na Busungu na Niyonzima anatarajiwa kuanza kwenye eneo la kiungo baada ya mchezo uliopita dhidi ya Medeama ya Ghana kuanzia benchi.
Katika hatua nyingine, kocha huyo alisema maandalizi yao yanakwenda vizuri na wachezaji wake wote wapo katika hali nzuri.

No comments:

Post a Comment