Monday 8 August 2016

WATANZANIA TUIOMBEE AMANI YA NCHI YETU

Image result for magufuli na mkewe katika ibadaRAIS John Magufuli ametembelea msikiti na makanisa yaliyopo Chato mjini mkoani Geita na kuendelea kuwasihi Watanzania kuombea amani na utulivu katika nchi, bila kujali tofauti za dini, makabila na kanda wanazotoka.
Rais alitoa ujumbe huo mara baada ya kusali ibada ya Jumapili katika Kanisa Katoliki la Bikira Maria Parokia ya Chato. Baadaye alitembelea Kanisa la Anglikana la Mtakatifu Stephano Parokia ya Chato, Kanisa la African Inland Church la Chato na kumalizia katika Msikiti wa Omar Bin-L-Khattab wa Chato.
Rais Magufuli alisema pamoja na Watanzania wote kuungana kuombea amani na utulivu, pia hawana budi kutekeleza kwa vitendo maandiko matakatifu ya Biblia yasemayo “Asiyefanya kazi na asile” kwa kuhakikisha kila mmoja anachapa kazi kwa juhudi na maarifa ili kuharakisha maendeleo ya Taifa.
“Ndugu zangu nawashukuru sana, muendelee kuliombea taifa hili, taifa letu ni la umoja, sisi wote ni Watanzania, tuendelee kumuomba Mola wetu, kudumisha amani yetu, kujenga umoja wetu kwa dini zote, makabila yote na vyama vyote, kwa sababu Mola wetu anatupenda sisi sote,” alisema Rais Magufuli.
Aidha, baada ya kuwasalimu waumini wa Kanisa Katoliki la Bikira Maria Parokia ya Chato, Rais Magufuli aliendesha harambee ya kuchangia ujenzi wa jengo jipya la kanisa hilo, ambapo Sh milioni moja zilikusanywa papo kwa hapo.
Tayari Rais Magufuli alishachangia ujenzi huo kwa kutoa Sh milioni moja Aprili 3, mwaka huu.
Alitoa wito kwa watu mbalimbali, kujitokeza kuchangia ujenzi wa kanisa hilo. Katika Msikiti wa Omar Bin-L-Khattab na makanisa ya Anglikana na African Inland, Rais Magufuli alichangia Sh milioni tano kwa kila moja kwa ajili kuendeleza na kukarabati majengo.
Kitwanga aandaa Ibada
Katika hatua nyingine, Watanzania wametakiwa kumuombea Rais Magufuli ili aweze kutekeleza vyema majukumu yake ya kitaifa na kuleta maendeleo endelevu nchini.
Pia wametakiwa kumgeukia Mungu kwa kulikubali neno lake, ambalo limeelezwa ni neno la uzima litakalowakomboa kutoka kwenye utumwa wa dhambi.
Hayo yameelezwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza, Askofu Yuda Thaddeus Ruwa’ichi alipokuwa akitoa mahubiri kwenye ibada maalumu ya kumuombea Rais Magufuli na familia ya Mbunge wa Misungwi, Charles Kitwanga (CCM) iliyofanyika nyumbani kwa mbunge huyo.
“Kwenye maisha, Mkristo ukiwa mwangalifu unayo fursa ya kuyaona maisha ya Mungu na utukufu wake,” alisema na kuongeza; “Niwaombe mbali na kuikumbuka familia hii ya Mheshimiwa Kitwanga kwa maombi, naomba tuendelee kumuombea Rais wetu mpendwa John Magufuli ili kusudi yale aliyoyapanga kuyatekeleza, ayatekeleze kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu,” alisema.
Alisema Rais kama Mkuu wa nchi, anayo majukumu mazito ya kuongoza nchi, ambapo alisema ni vyema wananchi kwa umoja wao wakawa wanamkumbuka kwenye maombi.
Aliwataka wanadamu kumfuata Kristo kwa sababu ni utimilifu wa torati na utimilifu wa manabii na unabii, ambapo pia alitumia fursa hiyo kuwataka Watanzania na Wakristo watambue kuwa neno la Mungu, si neno la udaku wala kuzusha, bali ni injili bora ya Yesu Kristo kwenye maisha yao.
“Watu wengi tuna utapiamlo wa kiroho kutokana na kutojihusisha na mambo ya kiroho,” alisema na kuwataka Wakristo nchini na Watanzania wawe tayari kumpokea Yesu Kristo kwenye maisha yao.
Kwa upande wake, Kitwanga alisema kuwa ameamua kufanya ibada hiyo kwa lengo la kumuombea Rais Magufuli ili aendelee kutekeleza vyema majukumu yake kama Rais wa nchi.
Aliwataka wananchi wa Misungwi, watambue kuwa uchaguzi umekwisha na kwamba kilichobaki kwao ni kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za maendeleo ili kuijenga Misungwi mpya yenye maendeleo.
Alimshukuru Askofu Ruwa’ichi kwa kuendesha ibada maalumu hiyo, ambayo imeleta faraja kubwa ndani ya familia yake na wananchi wa Misungwi.
Meya awapasha madiwani
Wakati hayo yakijiri, Watanzania wameombwa kutomchosha Rais Magufuli kwa kutaka kufanyiwa mambo madogo ya maendeleo, ambayo yako ndani ya uwezo wao, badala yake wajenge tabia ya kujitoa na kutumia uwezo wao katika kujiletea maendeleo.
Rai hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Meya wa Ilemela, Renatus Murunga wakati alipokuwa akijibu madai ya madiwani kwenye kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika mjini hapa.
Alisema ipo tabia iliyojengeka miongoni mwa Watanzania na wanasiasa, kudhani kuwa kila jambo la maendeleo ikiwemo ujenzi wa shule za msingi na sekondari, utafanywa na Rais Magufuli.
“Shule za msingi ni zetu wenyewe si za Rais Magufuli, kila mtu, mtumishi wa umma, kiongozi wa kisiasa ana wajibu wa kuhakikisha mtoto wake anapata elimu, haiwezekani sasa mwananchi akae akisubiri msaada kutoka serikalini kwa ajili ya maendeleo yake,” alifafanua.
Alisema kwa upande wa maendeleo, Serikali haina uwezo wa kufanya kila kitu na kwamba wananchi nao wana mchango wao katika kuiletea nchi maendeleo, ambapo alimtaka kila Mtanzania awajibike kwenye eneo lake.
“Haiwezekani Serikali ilipe mishahara ya watumishi, ichimbe matundu ya vyoo, itengeneze madawati, hebu tujenge tabia ya kuwekeza kwenye shughuli za maendeleo na elimu kwa ajili ya watoto wetu,” aliongeza.
Alisema ipo tabia ya baadhi ya watu, kugeuza mambo ambayo yamo ndani ya uwezo wao na kuyaona kama changamoto kwao, wakisubiri msaada kutoka Serikali Kuu wakati yanaweza kutatuliwa na wao wenyewe.
“Badala ya kumtegemea Rais Magufuli ambaye ana majukumu ya kitaifa na kimataifa, mambo mengine tuyafanye sisi wenyewe, hivi kweli hata ujenzi wa matundu ya vyoo tumsubiri Rais aje atujengee,” alihoji.
Aliwataka madiwani waendelee kuwahamasisha wananchi kwenye maeneo washiriki kikamilifu kwenye shughuli za uzalishaji mali na maendeleo, ambapo alisisitiza kuwa suala la maendeleo halina ushabiki wa kisiasa.

No comments:

Post a Comment